Wednesday, 3 September 2014

Barcelona yaanza LALIGA kwa makeke, Messi ang’ara

     
Timu ya soka ya Barcelona ya Uhispania imeanza msimu mpya wa ligi kuu ya soka nchini humo al-maarufu LALILGA kwa ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya timu ya Elche. Timu hiyo ambao kwa sasa inanolewa na mkufunzi Luis Enrique ikicheza katika uwanja wake wa nyumbani wa Camp Nou ilionekana ikiwa na sura nyingi ngeni baada ya kuwasajili makinda kadhaa akiwemo Munir El Haddadi mwenye umri wa miaka 18 ambaye anaonekana kuwa tishio katika safu ya ushambuliaji. Nyota wa timu hiyo Lionel Messi alipachika mabao 2 katika dakika za 42 na 63, huku bao la tatu likitiwa kimiani na kinda Munir El Haddadi katika dakika ya 46 ya mchezo. Mambo yalionekana yangewavurugikia Barcelona baada ya mlinzi wake Javier Mascherano kulimwa kadi nyekundu katika dakika ya 43 ya kipindi cha kwanza. Hata hivyo pengo la Mascherano halikuwa kikwazo kwa Barcelona kung’ara na kuibuka na ushindi katika mchezo huo. Katika mechi nyingine za ufunguzi zilizochezwa jana Celta de Vigo imeibamiza Getafe mabao 3-1, Villareal imeitandika Levante viboko viwili bila majibu, Granada imeipeleka mchakamchaka  Deportivo de la Coruna kwa kuifunga mabao 2-1, Malaga imeiadhibu Athletic bao 1 kwa yai, huku Sevilla na Valencia zikitoshana nguvu kwa kufungana bao 1-1, matokeoa ambayo yalitawala pia mchezo kati ya Almeria na Espanyol. Ligi hiyo itaendelea tena leo ambapo Real Madrid watamenyamana na Cordoba huku mabingwa watetezi Atletico Madrid wakiwa wageni wa Rayo Vallecano.

No comments:

Post a Comment