Wednesday, 3 September 2014

MIDO LA UKWELI JONAS GERARD MKUDE SASA FITI KABISA, KUINGIA KAMBINI JUMTATU ZENJI SIMBA SC


KIUNGO wa kimataifa wa Tanzania, Jonas Gerard Mkude ameanza mazoezi mepesi kuelekea kurejea uwanjani baada ya kupona maumivu ya goti, aliyoyapata Juni mwaka huu. Mkude aliumia akiichezea timu ya taifa, Taifa Stars katika mchezo wa kirafiki nchini Botswana mjini Gaborone na baada ya vipimo na tiba, akatakiwa kupumzika kwa wiki sita. “Nipo fiti kabisa kwa sasa, nimeanza mazoezi ya viungo chini ya usimamizi wa Daktari na ninaendelea vizuri,”amesema kiungo huyo wa Simba SC. Mchezaji huyo mahiri wa sehemu ya kiungo wa ulinzi, amesema Jumatatu anatarajia kujiunga na wachezaji wenzake wa Simba SC kambini visiwani Zanzibar. 
Anarudi; Kiungo Jonas Mkude ameanza mazoezi mepesi na Jumatatu anaingia kambini Simba SC
Atakaporejea, mtihani wake wa kwanza Mkude utakuwa kujifua kurudi katika kiwango chake na baada ya hapo amshawishi kocha Mzambia, Patrick Phiri kumrejesha kwenye kikosi cha kwanza. Phiri amerejea Simba SC kipindi ambacho Mkude ni majeruhi, hivyo hajawahi kufanya naye kazi na tayari amemuamini kiungo mpya Mrundi, Pierre Kwizera katika nafasi ya kiungo mkabaji. Lakini bado mbele ya wana Simba SC, Mkude ndiye mchezaji anayekubalika zaidi kuzungusha dimba la chini- hivyo kiungo huyo atalazimika kumshawishi na kocha Phiri akubaliane naye.   Mkude anaweza kukosa mechi za mwanzo za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, ambayo inatarajiwa kuanza Septemba 20, mwaka huu, Simba SC ikifungua dimba na Coastal Union Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam Septemba 21. Mabingwa watetezi, Azam FC wataanza na Polisi Morogoro Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam Septemba 20, mwaka huu, wakati Yanga SC waliomaliza nafasi ya pili wataanza na Mtibwa Sugar Uwanja wa Jamhuri, Morogoro siku hiyo. Washindi wa tatu, Mbeya City wataanza na JKT Ruvu ya Pwani, Uwanja wa Sokoine, Mbeya Septemba 20. Mechi nyingine za ufunguzi za Ligi Kuu zitakuwa kati ya Stand United watakaoikaribisha Ndanda ya Mtwara Uwanja wa Kambarage, Shinyanga, Mgambo JKT wataikaribisha Kagera Sugar Uwanja wa Mkwakwani, Tanga na Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Prisons Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

No comments:

Post a Comment